Waziri wa Afya Mhe. Jenista Mhagama amesema Hospitali Maalum ya Tiba Magonjwa Ambukizi kibong’oto inatarajiwa kuwa Taasisi ya Magonjwa Ambukizi ambayo itakwenda sambamba na uimarishaji wa mifumo ya huduma za tiba ya magonjwa hayo.
Waziri Mhagama amesema hayo Machi 1, 2025 alipofanya ziara katika Hospitali ya Kibong’oto kwa lengo la kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ambayo Serikali imetoa fedha ikiwa ni pamoja na eneo la uzalishaji wa gesi tiba na ununuzi wa mashine za kisasa za kuchomea taka.
“Tumejipanga kwenye Sekta ya Afya, pamoja na huduma nyingine za afya za kibobezi, tunataka kuuthibitishia ulimwengu kwamba hata kwenye eneo hili la magonjwa ambukizi kama nchi tumejizatiti vizuri kwa kuhakikisha mifumo yetu ya tiba iko imara,” amesema Waziri Mhagama.
Amesema, magonjwa hayo ambukizi yanaweza kuibuka mahala popote katika nchi, hivyo kwa uwekezaji mkubwa uliofanywa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan unaiwezesha Tanzania kupambana na magonjwa hayo kwa kuzingatia utaratibu na mifumo ya afya iliyopo.
“Kwa hiyo hapa sasa kitakuwa ni kituo cha umahiri katika eneo hilo la magonjwa ambukizi, ninafurahi niliolpokuja kuzindua Bodi tulikubalia ni lazima tuwe na mpango mkakati unaotekelezeka, ambao utatufikisha kwenye malengo endelevu na sasa naona utekelezaji wake umeanza,” amesema Waziri Mhagama.
Aidha Waziri Mhagama amesema Serikali imewekeza zaidi zaidi ya Shilingi Milioni 550 kwa ajili ya kujenga sehemu maalum ya kuchomea taka pamoja na ununuzi wa mashine maalum ya kisasa ambao una uwezo wa kuteketeza taka zaidi ya Kg 400 kwa saa moja katika eneo hilo.
“Mashine hizi ni zile za kisasa na za hali ya juu ambazo hazina athari za kiafya kwa wananchi pamoja na hifadhi za mazingira kwa kuwa moshi unaotoka hapo ni moshi mweupe ambao ni salama kwa wagonjwa na mazingira yetu kwa ujumla,” amesema Waziri Mhagama.
Pia, Waziri Mhagama amesema Serikali kupitia Wizara ya Afya imewekeza zaidi ya Bilioni 1.6 kwa ajili ya kutengeneza mradi wa kuzalisha gesi tiba ambao mradi huo umeshakamilika na kuanza kufanya kazi katika Hosoitali hiyo, ambao umesaidia kuokoa fedha za kuagiza gesi hiyo kutoka nje.
Waziri Mhagama ameupongeza uongozi wa hospitali hiyo kwa usimamizi mzuri ikiwa ni pamoja na kukarabati majengo ya zamani kama jengo la Utawala, baada ya Serikali kutoa kiasi cha Shilingi Bilioni 1.5 na kuwataka waendelee na kasi hiyo.