Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Mhe. Stanslaus Haroon Nyongo (Mb), amezindua rasmi Jengo la Hazina Mkoa wa Geita kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), na kusisitiza umuhimu wa watanzania kuwa na nidhamu ya fedha, kukopa kwa ajili ya mahitaji yenye tija na kuchukua mikopo kwa ajili ya shughuli za uzalishaji mali ili kuepukana na janga la mikopo umiza.
Aidha, Mhe. Nyongo, imeiagiza Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na ofisi zote zinazoshughulika na usimamizi wa sekta ya fedha na Kamati zote za Ulinzi na Usalama kufuatilia kwa ukaribu taasisi zote zinazotoa mikopo nchini.
Alisema kuwa changamoto ya mikopo umiza imekuwa ni ya muda mrefu na inaendelea kurudisha nyuma maendeleo ya wananchi wa kawaida na kwamba ni lazima hatua zichukuliwe haraka kukomesha tatizo hilo.
“Naelekeza kuchukua hatua kali dhidi ya wanaotoa huduma za fedha bila leseni na kuwanyanganya leseni wote watakaobainika wanatoa mikopo bila kuzingatia mashariti ya leseni.
Aidha, alitoa onyo kwa watu binafsi na kampuni zinazojihusisha na utoaji wa mikopo ya namna hiyo kuacha mara moja kwani jambo hilo linarudisha nyuma wananchi.
Alieleza kuwa uwepo wa Ofisi za Hazina Ndogo mkoa wa Geita itawapunguzia wananchi kutembea umbali mrefu na gharama ili kupata huduma pamoja na kuwasaidia kupata elimu ya kifedha kutoka kwa watumishi wa Hazina.
Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Utawala ba Rasilimali watu wa Wizara ya Fedha, Bw. Lusius Mwenda, amesema Jengo hilo lina Ofisi 14 zitakazotumika na watumishi 50 na litatumiwa na Idara mbili ambazo ni Idara ya Usimamizi wa Mali za Serikali na Hazina Ndogo Mkoa wa Geita pamoja na Ofisi ya Takwimu Mkoa wa Geita.
“Jengo hili litaboresha mazingira ya kazi kwa watumishi wetu, na wateja wetu, itapunguza gharama za uendeshaji wa Ofisi hususani kukodi kwa maana ya kulipa pango”, amesema Mwenda.
Mshauri Elekezi wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), Bi. Amina Lumuli, alisema kuwa mradi wa Jengo la Hazina Ndogo Geita umetekelezwa na Mkandarasi Masasi Construction Co. Ltd. pamoja na TBA ambaye ni Mshauri Elekezi.
“Mradi ulianza Juni 30, 2023 na kukabidhiwa Desemba 03, 2024 ambapo mradi huu ulikuwa wa miezi 15, gharama za mradi ni sh bilioni 4.37 pamoja na VAT gharama za Mshaur Elekezi ni sh milioni 269″, alisema Bi. Lumuli.
Mwakilishi wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti na Mbunge wa Meatu, Mhe. Leah Komanya alisema kuwa Serikali itaendelea kuiwezesha Ofisi ya Mweka Hazina ili kutoa mafunzo kwa wahasibu wa Ofisi za Hazina Ndogo.