Bohari ya Dawa (MSD) imepongezwa kwa kuimarisha mnyororo wa ugavi wa bidhaa za afya mkoani Kagera, ambao umepunguza malalamiko ya upungufu wa bidhaa za afya mkoani humo.
Pongezi hizo zimetolewa hapo Januari 6 mwaka 2025 na Katibu Tawala wa Mkoa huo Stephen Ndaki, wakati akizungumza na ujumbe maalum kutoka MSD uliomtembelea ofisini kwake, ukiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya MSD Bi. Rosemary Silaa, ikiwa ni ziara maalum ya kuadhimisha miaka 30 ya MSD.
Ndaki amebainisha kuwa maboresho ya huduma za MSD yamesaidia kuondoa kero na malalamiko ya mara kwa mara yaliyokuwepo miongoni mwa jamii na wateja juu ya uhaba wa Dawa vituoni, hivyo kupelekea kuimarika kwa hali utoaji wa huduma za afya Mkoani humo.
Ameongeza kwamba, mbali na kuimarika kwa utoaji huduma, hivi sasa uelewa wa majukumu ya MSD na jinsi inavyofanya kazi zake, umeongezeka miongoni mwa viongozi hivyo kuondoa kasumba ya kutupiana lawama juu ya ununuzi ya bidhaa za afya, baina ya MSD na Wateja wake, kwani viongozi wote ndani ya Mkoa huo wamejengewa uelewa.
“Hapo mwanzo kulikuwa na kelele sana kutoka vituoni kwamba tumelipa lakini MSD hajaleta, hatahivyo kwa siku za hivi karibuni malalamiko hayo yemeondoka, na uelewa juu ya mnyororo wa bidhaa za afya umeongezeka mpaka kwa viongozi, hivyo tuwapongeze kwa maboresho” Alisema Ndaki
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya MSD, Bi. Rosemary Silaa, ameeleza namna MSD ilivyopitia katika vipindi tofauti, na jinsi ilivyojizatiti kuboresha huduma zake, ili kupunguza, ama kuondoa kabisa changamoto chache zilizoukabili mnyororo wa bidhaa za afya.