Mtanzania Lydia Charles Moyo, amekuwa mmoja kati ya washindi sita waliotambuliwa kwa Tuzo ya Shirika la Kimataifa la Global Citizen mwaka 2024, ikionyesha juhudi za vijana ulimwenguni katika kuleta mabadiliko. Kwa mujibu wa taarifa, uthabiti wake usio na kifani katika kukabiliana na umasikini na kuwezesha kiuchumi kwa wasichana na wanawake vijana ndiyo umeleta utambuzi huu wenye heshima duniani, na kumweka pamoja na kikundi cha vijana wachache kinachong’ara miongoni mwa mamilioni ulimwenguni kote.
Kwa mujibu wa tovuti ya shirika la Her Initiative ambalo Lydia Moyo ni Mkurugenzi na mwanzilishi wake, shirika hilo lilianzishwa miaka mitano iliyopita. Kupitia shirika hili linaloongozwa na wanawake vijana, Lydia hutekeleza miradi inayolenga kuwawezesha kifedha wasichana na wanawake vijana, kuchagiza matumaini na fursa mahali ambapo wasichana na wanawake walikata tamaa.
Akizungumzia utambuzi huo, Lydia anawashukuru timu ya Her Initiative, pamoja na washirika, wafadhili, na wafuasi wa kazi zake, wote wa ndani ya Tanzania na kimataifa. “Tuzo hii inamaanisha mengi kwangu na kazi tunayofanya na shirika la Her Initiative. Inathibitisha uimara na azimio la wanawake na wasichana vijana, ambao wana ndoto na malengo makubwa na wanafanya kazi kwa bidii ili kuboresha siyo tu maisha yao binafsi, bali pia ya jamii zao,” anasema.
Washindi wa Tuzo ya Global Citizen mwaka 2024 watatambuliwa wakati wa mkutano wa ‘Global Citizen NOW’ mnamo Mei 1 na 2 huko New York, Marekani. Global Citizen ni shirika la utetezi na uchechemuzi la kimataifa linalopigania kumaliza umaskini.
Kwa msaada wa jamii ya kimataifa ya watetezi wa kila siku wanaopaza sauti zao na kuchukua hatua, juhudi zao zinapata nguvu kupitia kampeni na matukio yanayokusanya viongozi katika muziki, burudani, sera za umma, vyombo vya habari, hisani, na sekta ya biashara.