Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika Mh.Lord Collins amevutiwa na mpango wa nchi ya Tanzania kuandaa mkakati maalum wa uongezaji thamani madini nchini Tanzania na kuahidi kwamba Uingereza itatoa ushirikiano katika kusaidia eneo la uongezaji thamani madini hayo ndani ya nchi.
Hayo yamesemwa leo wakati wa kikao kati ya Mh. Lord Collins na Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde kilichofanyika leo Jijini Dar es salaam.
“Tanzania na Uingereza zina ushirikiano wa muda mrefu katika maeneo mengi ya kiuchumi ikiwemo sekta ya Madini.
Nimevutiwa na mkakati wa Tanzania wa kuongeza thamani ndani ya nchi, mkakati ambao Uingereza tunauunga mkono na tupo tayari kuwezesha utekelezaji wake kupitia Mradi wa “Manufacturing Africa“ ambapo ya pauni 2.1 bilioni zimetengwa kusaidia nchi 6 za Afrika,ikiwemo Tanzania,kutengeneza bidhaa za kati na za mwisho kupitia madini“ Alisema Lord Collins
Akizungumza katika Kikao hicho,Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde amesema Tanzania inayo mkakati wake maalum wa uongezwaji thamani madini ili kuongeza manufaa makubwa zaidi kwa nchi kupitia sekta ya madini,ambapo kwa sasa madini yanapaswa kuchakatwa na kuongezwa thamani nchini.
Serikali imetenga eneo maalum la ujenzi wa viwanda vyakuongeza thamani wilayani Kahama,Mkoani Shinyanga kwa lengo la kuvutia uwekezaji katika eneo hili.