TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imefanikiwa kuokoa kiasi cha Milioni 76,048,459.1 baada ya kuwafikisha mahakamani waliokuwa watumishi wa umma kwa tuhuma za ubadhirifu na ufujaji wa Fedha za Umma katika wilaya za Kilindi, Korogwe na Tanga Jiji.
Tuhuma ambazo zilikuwa zinawakabili ni kutokuwasilisha fedha ambazo ni mapato ya Serikali yaliyokusanywa kwa mfumo wa POS na kuzitumia kwa manufaa yao pasipo kuwasilishwa sehemu husika kwa taratibu zilizowekwa.
Hayo yalisemwa leo na Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Tanga Ramadhani Ndwatah wakati akitoa taarifa ya utendaji wa taasisi hiyo kwa kipindi cha miezi miwili kuanzia mwezi Octoba hadi Desemba mwaka 2024.
Ambapo alisema kwamba baada ya kufikishwa mahakamani Jamhuri ilishinda kesi hiyo ambapo waliamriwa na mahakama kurejesha fedha kiasi hicho kwa mchanganuo mbalimbali.
Aidha alisema kwa wilaya ya Kilindi katika ufuatiliaji wa Jamhuri kushinda kesi za hujumu uchumi namba 13,2023,11/2023 na 06/2024 dhidi ya watumishi ambao walishtakiwa kwa ubadhirifu kufuatia kutokuwasilisha fedha ambazo ni mapato ya Serikali yaliyokusanywa kwa mfumo wa POS na kuzitumia kwa manufaa yao pasipo kuwasilishwa sehemu husika kwa taratibu zilizowekwa.
“Fedha kiasi cha Sh Milioni 58,678,780.00 zilirejeshwa na watumishi hao kwa amri ya mahakama sambamba na adhabu nyengine “Alisema
Mkuu huyo wa Takukuru Mkoa alitaja wilaya nyengine kuwa wilaya ya Korogwe ambapo kiasi cha Milioni 9,198,045.31 ambazo ni mapato ya Serikali yaliyokusanywa kwa mfumo wa POS zilirejeshwa kwa amri ya mahakama kufuatia Jamhuri kushinda kesi za uhujumu Uchumi namba 09/2023 na 10/2023 dhidi ya watuhumiwa.