Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa mgeni Rasmi wa mkutano huo.
Tanzania itakuwa mwenyeji wa Mkutano na Maonesho ya 11 ya Petroli ya Afrika Mashariki (11TH East African Petroleum Conference and Exhibition – EAPCE’25), utakaofanyika tarehe 5 hadi 7 Machi 2025 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam. Kauli mbiu ya Mkutano huu, ni “Kufungua Fursa za Uwekezaji katika Nishati: Mchango wa Rasilimali za Mafuta katika Kupata Nishati ya Uhakika kwa Maendeleo Endelevu ya Afrika Mashariki,”. Mkutano huu utafunguliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan. Mkutano huu utatanguliwa na semina kuhusu masuala ya nishati safi ikiwemo nishati safi ya kupikia na matumizi ya gesi kwenye magari (CNG) itakayofanyika tarehe 4 Machi, 2025.
Mkutano wa EAPCE’25 utawaleta pamoja washiriki zaidi ya 1000, wakiwemo watunga sera, viongozi wa Serikali kutoka nchi mbalimbali ikiwemo nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, wawekezaji wa kimataifa na wa ndani. Akizungumza wakati wa mkutano na vyombo vya habari, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati Mha. Felchesmi Mramba alisema kuwa “Mkutano huu wa EAPCE’25 utatoa nafasi ya kujadili mchango wa rasilimali za mafuta na gesi asilia katika mchanganyiko wa nishati kwa maendeleo endelevu ya Afrika Mashariki na fursa za uwekezaji zilizopo katika sekta ya mafuta na gesi Afrika Mashariki”. Aidha, Mhandisi Mramba alieleza kuwa mada mbalimbali kutoka kwa wataalam na wabobezi katika sekta ya mafuta na gesi zitatolewa zikiwemo utafutaji na uendelezaji wa mafuta na gesi katika nchi za Afrika Mashariki, fursa za uwekezaji katika mnyororo wa thamani wa mafuta na gesi, dhana ya kuelekea nishati safi, masuala ya mazingira, miundo ya kisera, kisheria na kiudhibiti katika mafuta na gesi na kadhalika. Vilevile, mkutano utahusisha maonesho ya bidhaa na huduma kutoka kampuni mbalimbali katika mnyororo wa thamani wa mafuta na gesi asilia.
Aidha, Mhandisi Mramba alieleza kuwa Mkutano wa EAPCE’25 unafanyika katika wakati muhimu baada ya Tanzania kuwa mwenyeji wa mkutano wa wakuu wa nchi za Afrika kujadilia masuala ya nishati. Katika mkutano wa Mission 300 nchi za Afrika zilikubaliana kuweka Mpango Mahususi wa Taifa wa Nishati kwa kipindi cha miaka mitano 2025-2030 ambapo kwa Tanzania mpango wetu ni kuunganisha watumiaji wa umeme kufikia 75%, kuongeza kiwango cha upatikanaji umeme kufikia 100% na kuwezesha matumizi ya nishati safi ya kupikia kufikia 75% ifikapo mwaka 2030. Mhandisi Mramba alieleza kuwa “ili kufikia malengo haya tunahitaji kutumia rasilimali zetu za asili ikiwemo za mafuta na gesi ili kuchangia katika upatikanaji wa nishati ya uhakika ikiwemo nishati safi ya kupikia”.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kikanda ya maandalizi ya EAPCE’25 ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu kutoka Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio aliongeza kuwa Mkutano huu unahusisha pia ziara za kitaaluma katika maeneo ya kijiolojia katika nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ili kuwapa washiriki mtazamo wa vitendo kuhusu sekta. Dkt. Mataragio alisema “Ziara hizi zitatoa fursa ya kuona miradi inayoendelea na mipango ya baadaye, jiolojia katika nchi za Afrika Mashariki na hivyo kuwawezesha wawekezaji na wadau kubaini fursa za biashara na ushirikiano katika sekta ya nishati katika ukanda wetu”.
Kuhusu utaratibu wa kushiriki katika mkutano wa EAPCE’25, Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi, Mhandisi Joyce Kisamo alisema “tunawahimiza makampuni na wadau mbalimbali wa sekta ya mafuta na gesi kujiandikisha kushiriki katika mkutano huu na pia kutumia nafasi hii kutangaza bidhaa na huduma zao kupitia maonesho”.
Kwa taarifa zaidi kuhusu Mkutano wa EAPCE’25 pamoja na kujisajili kushiriki, tafadhali tembelea www.eapce25.eac.int au mitandao ya kijamii kama mtandao wa X na Instagram kwa jina la: @eapce25
Mkutano wa EAPCE’25 umewezeshwa na umedhaminiwa na wadau mbalimbali waliojitolea kusaidia maendeleo ya sekta ya mafuta na gesi katika Afrika Mashari