Serikali ya Awamu ya Sita kupitia wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini RUWASA imetoa zaidi ya shilingi Millioni 271 kwaajili ya uboreshaji wa mradi wa maji wa Ruaha Mbuyuni wilayani Kilolo, mradi ambao unaenda kuondoa adha ya upatikanaji wa maji safi na salama.
Akizungumza wakati akishuhudia zoezi la utiaji saini, uboreshaji wa mradi wa maji wa Ruaha Mbuyuni Wilayani Kilolo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa Serukamba ameishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha hizo zinazoenda kumaliza changamoto ya maji safi ma salama katika eneo hili.
Serukamba ameongeza kwa kuwasisitiza wakandarasi walio saini mkataba huo kufanya kazi kwa Haraka na kwa ubora ili kuwezesha Wananchi wa kijiji cha Ruaha Mbuyuni na Msosa kupata huduma ya maji safi na salama.
Wakala wa Maji na Usafi wa mazingira Vijijini (RUWASA) wameahidi kuusimamia Ipasavyo mradi huo ili uweze kukamilika Kwa Wakati na yasijirudie makosa kama ya mwanzo.
Kwa upande wao Wananchi wa Kijiji Cha Ruaha Mbuyuni wameishukuru Serikali Kwa kuwasadia kuboresha mradi huo wa Maji ambapo wamesema utakwenda kuwa Mkombozi kutokana na adha kubwa wanayoipitia kwasasa ya ukosefu wa maji safi na salama suala linapelekea kukwamisha shughuli zao za Kiuchumi.
Uboreshaji huo wa mradi wa maji wa Ruaha Mbuyuni utahudumia Vijiji Viwili vya Msosa na Ruaha Mbuyuni vyenye jumla ya watu wapatao 34,028.