Kutokana na ukosefu na uharibifu mkubwa wa Miundombinu ya Barabara Ilala, zaidi ya Shilingi bilioni 10.7 kutoka katika mapato ya Halmashauri zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara Jiji la Dar es Salaam kwa kiwango cha lami.
Hayo yamebainishwa leo na Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam Ndugu Omary Satura kwenye hafla fupi ya utiaji saini mikataba ya ujenzi wa barabara 10 kati ya Jiji la Dar es Salaam na wakandarasi wanaoenda kutekeleza miradi hiyo.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo Mkuu wa Wilaya ya Ilala Edward Mpogolo amewataka Wakandarasi kuwa waadilifu kwa kuhakikisha wanakamilisha miradi kwa wakati huku akiwasisitiza washirikiane katika kazi ili kuleta matokeo yenye tija kwa maslahi ya Wananchi.
Sambamba na hilo Dc Mpogolo ametoa pongezi kwa Mstahiki Meya na Madiwani kwa usimamizi mzuri wa miradi huku akimpongeza Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam kwa kushirikiana na watendaji wa Jiji kwa kasi ya ukusanyaji wa mapato ambao umekua chachu ya kuleta maendeleo kwa wananchi wa Jiji la Dar es Salaam.
Kwa upande wake Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam Omary Kumbilamoto amemshukuru Rais Wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa fedha anazotoa kwa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kwaajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo huku akitoa wito kwa Wakandarasi kutekeleza miradi kwa wakati uliopangwa ili waweze kutimiza adhma ya Rais ya kuhakikisha huduma bora zinawafikia wananchi kwa wakati.