Imeelezwa kuwa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani kwa mwaka 2025 yatakuwa kwa namna ya kipekee yakibeba sura ya kipekee kwa kuwa yanaambatana na miaka 30 ya utekelezaji wa Azimio la ulingo wa Beijing (1995).
Hayo yamebainika jijini Dar Es Salaam Februari 03, 2025 wakati wa Mkutano wa Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima na waandishi wa Habari kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani kwa mwaka 2025.
Waziri Dkt. Gwajima amesema, kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani tarehe 8 Machi, 2025 kitafanyika Kitaifa Mkoani Arusha na awali, kilele hicho kitatanguliwa na maadhimisho katika ngazi ya Mikoa nchi nzima ili kuwa na ushiriki wa Wanawake na jamii kwa wingi zaidi ambapo, kwenye siku ya kilele, Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
“Katika mkutano huo wa Beijing yalifikiwa maazimio ambayo Tanzania kama nchi mwanachama wa Umoja wa Mataifa imeendelea kutekeleza. Mwaka huu ni wa thelathini (30) tangu utekelezaji ulipoanza, hivyo mataifa yatatumia maadhimisho haya kutathimini utekelezaji wa Azimio la Ulingo wa Beijing ikiwa pamoja na kuweka mikakati endelevu ya utekelezaji” amesema Waziri Dkt. Gwajima
Ameongeza kuwa wiki ya maadhimisho hayo Wizara, Taasisi za Umma na Binafsi na Makampuni zitatoa huduma mbalimbali kwa wananchi. Vilevile kutakuwa na maonesho ya bidhaa za wajasiriamali mbalimbali hivyo ametoa rai kwa wananchi kujitokeza katika maeneo yao kupata huduma na kununua bidhaa mbalimbali.