Waziri wa Afya, Jenista Mhagama, amesema ujenzi wa ghala la kuhifadhi bidhaa za afya la Bohari ya Dawa Kanda ya Dodoma lenye ukubwa wa mita za mraba 7,200, litakalogharimu zaidi ya Tsh. bilioni 23.7 umefikia 95%.
Mhagama amesema hayo leo February 6, 2025 wakati akikagua ujenzi wa ghala hilo, Jijini Dodoma ambapo amesema ghala hilo linatarajiwa kuzinduliwa rasmi mwezi Aprili ambapo uzinduzi huo utaenda sambamba na uzinduzi wa ghala jingine Mkoani Mtwara linalogharimu zaidi ya Tsh. bilioni 18.
“Tunakwenda kuweka maghala mengine katika Mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Songea, Chato, Iringa, Moshi na Arusha ikiwa ni muendelezo wa mikakati ya kuhakikisha mfumo mzima wa mlolongo wa usambazaji wa bidhaa za afya zinapatikana kwa wakati, ubora unaotakiwa na kuhifadhiwa katika mazingira mazuri
Waziri Mhagama amesema kuwa Sekta ya Afya ina jukumu la kutoa huduma bora kwanza lakini ili kufanya hivyo inawapasa MSD kufanya biashara na kuzidi kuongeza mapato yake ili kuendesha shughuli zinazofanywa na bohari hiyo na kutimiza lengo la kutoa huduma bora kwa Wananchi.
“Hatuwezi MSD kuendelea kuitegemea Serikali ni lazima tuiondolee mzigo Serikali wakati huohuo tufanye mambo makubwa yatakayoifanya Serikali kutambulika kimataifa zaidi, kwa MSD kujitengenezea program mpya za kisasa zinazohusika kwenye ukanda wa Afrika na kujiuza ukanda wa SADC,”