Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema Serikali itahakikisha inajiimarisha katika kukuza uchumi wake kwa kutumia rasilimali zilizopo ili kuweza kumudu kutekeleza maeneo yote muhimu yakiwemo ya sekta ya afya, elimu na maji.
Ameyasema hayo leo Alhamisi, Februari 6, 2025 wakati akijibu swali la Mbunge wa Mbozi, George Mwanisongole katika kipindi cha maswali kwa Waziri Mkuu Bungeni jijini Dodoma “Tanzania itatumia vyanzo vya fedha na mapato vilivyowasilishwa Bungeni ili vipangiwe kazi ili kujazia maeneo yaliyopungua”
Mbunge huyo alitaka kujua Serikali inajipangaje na mabadiliko ya sera za nje ya nchi ya Marekani ambayo yanakwenda kuathiri utekelezaji wa sera za elimu, afya na uchumi hususan miradi ya maendeleo inayofadhiriliwa USAID.
”Uwezo tunao, tunazo maliasili, tunazo rasilimali, kazi ambayo tunayo ni Watanzania kushirikiana kuhakikisha tunatumia maliasili na rasilimali tulizonazo kujenga uchumi wa ndani kuwezesha mipango na bajeti iweze kutekeleza haya.”
Amesema Tanzania inaheshimu sera za mambo ya nje na inatekeleza mikataba kwa mujibu wa sera hizo kama ilivyokubaliana na nchi husika katika maeneo mbalimbali. ”Tumeanza kuona nchi zenye uwezo mkubwa ikiwemo Marekani ikibadilisha sera zao na mabadiliko yake yanathiri baadhi ya nchi, kwetu sisi ni muhimu kuzingatia sera za nje na kuzitekeleza kama tulivyokubaliana.”