Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Ireland zimesaini hati ya makubaliano katika Sekta ya Afya ili kuendeleza ushirikiano uliopo ikiwemo kubadilishana uzoefu baina ya watalaam katika nchi hizo mbili, kufanya utafiti wa matibabu pamoja na kusaidia katika hatua za lishe kwa kupunguza udumavu wa watoto.
Makubaliano hayo yamesainiwa leo Februali 19, 2025 na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Dkt. Seif Shekalaghe na Mkurugenzi wa ‘Wellbeing and Global Health’ Dkt. Philip Crowley ambayo yameshuhudiwa na Waziri wa Afya Mhe. Jenista Mhagama pamoja na Balozi wa Ireland nchini Tanzania Mhe. Nicola Brennan.
“Napenda kuishukuru Ireland kwa kuwa mshirika muhimu katika uboreshaji wa huduma za afya nchini Tanzania, Serikali yetu chini Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, itaendelea kushirikiana na watendaji wa Ireland na watendaji wa huduma za afya katika kuboresha Sekta ya Afya kwa ustawi wa wananchi wa Tanzania,” amesema Dkt. Shekalaghe