Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene amewataka Wajumbe wa Bodi ya Kima cha Chini cha Mshahara kuwasilisha mapendekezo ya Kima cha chini cha mshahara yanayochozingatia hali halisi ya maisha na maslahi ya wafanyakazi ili kuepuka migogoro na kushuka kwa morali ya wafanyakazi, tija na uzalishaji.
Mhe. Simbachawene amesema hayo leo jijini Dodoma wakati akizindua Bodi ya Kima cha Chini cha Mshahara katika Utumishi wa Umma.
Mhe. Simbachawene amesema Kima cha Chini cha Mshahara ni suala muhimu sana na lisiposhughulikiwa vizuri linaweza kusababisha migogoro isiyo ya lazima na hivyo kuzorotesha uchumi na maendeleo ya nchi kwa ujumla.
Ameongeza kuwa, Kima cha chini cha mshahara kisichozingatia hali halisi ya uchumi ni hatari katika maendeleo ya nchi hasa kutokana na ukweli kwamba kunaweza kusababisha kutokea kwa mfumuko wa bei, na kuongeza gharama za uendeshaji.
Waziri Simbachawene amesema Bodi ya Mshahara katika Sekta ya Umma ina jukumu la kufanya uchunguzi na kupendekeza kwa Waziri mwenye dhamana na masuala ya Utumishi wa Umma kuhusu Kima cha Chini cha Mshahara katika Sekta ya Umma, hivyo katika kutekeleza majukumu haya, Bodi ina wajibu wa kuzingatia maslahi ya nchi na mustakabali wa uchumi wa nchi wakati wa kutoa mapendekezo stahiki.
Kwa Upande wake, Mwakilishi wa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Uendelezaji wa Taasisi, Bw. Nolasco Kipanda amesema pamoja na uzinduzi wa bodi hiyo, Wajumbe watapatiwa mafunzo kwa ajili ya kujengewa uwezo zaidi na kupata uelewa kuhusu majukumu ya upangaji wa kima cha chini cha mshahara katika Utumishi wa Umma.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Kima cha Chini cha Mshahara katika Utumishi wa Umma, Bw. Mathias Kabunduguru amemuahidi Waziri Simbachawene kuwa watatekeleza majukumu yao kwa ufanisi na malengo yaliyokusudiwa katika kupendekeza na kutoa ushauri kwa ustawi wa nchi.