Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi Taifa Fadhili Rajabu Maganya ametahadharisha vyama pinzani kuwa Chama chao hakiendi kirahisi wala kuonea huruma mpinzani aliye dhaifu katika uchaguzi wa mwaka huu (2025) kwa kuwa wamejipanga kikamilifu kuendelea kushika dola.
Maganya ameeleza hayo mjini Makambako mkoani Njombe wakati akizungumza na wanachama wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mara baada kupokewa kwa ziara ya siku tatu mkoani humo.
“Tunataka tuwapige kweli kweli,hatuwezi kuchukua mambo kirahisi kwa hiyo tuwaambie vyama rafiki tunataka tutumie silaha nzito na za kisayansi kuhakikisha tunawashinda kitakatifu na hatutajali kwamba tutumie silaha gani,sisi tutatumia bomu kuua nzi”amesema Maganya
Amewataka wanaCCM kutokuwa na wasiwasi na kwenda kuisemea vizuri serikali kwa kuwa imetekeleza kikamilifu Ilani yao.
Aidha Maganya amesema Chama cha Mapinduzi hakikutaka kuchelewa kumtangaza mgombea wao wa Urais ili kuwa wanachama utulivu wa akili ili kufikilia namna ya kutekeleza Ilani nyingine ya uchaguzi ya mwaka 2025-2030.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi mkoa wa Njombe Gerlad Mpogolo amesema Chama hicho kinakwenda kupata ushindi mkubwa kutokana na ushirikiano walionao.
“Jumuiya zetu zote tuna mahusiano mazuri na kwa ushirikiano tulionao tunaamini kupata ushindi mkubwa”amesema Mpogolo
Deo Sanga (Jah People) ni mbunge wa jimbo la Makambako ambaye pia ni mwenyekiti wa CCM mkoa wa Njombe ametoa wito kwa wanaohitaji kutia nia kwenye nafasi mbalimbali ikiwemo Ubunge na Udiwani kutulia kufuata taratibu za Chama bila kuleta vurugu huku akibainisha kuwa yeye bado yupo katika jimbo hilo.