Serikali kupitia kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (TAMISEMI) Selemani Jafo imetoa maagizo kwa wakuu wa shule zote nchini kuhakikisha somo la michezo linafundishwa ipasavyo ili kuwaandaa vijana vyema.
Jafo ameyasema hayo jijini Dodoma katika kikao cha pamoja kati ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Ofisi ya Rais TAMISEMI pamoja na Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia kilichoandaliwa na Wizara ya Habari ambacho kilijadili namna ya kuboresha michezo katika shule za msingi na sekondari.
Aidha, Jafo ameziagiza Halmashauri zote nchini kutenga maeneo kwa ajili ya shughuli za michezo, huku akiagiza Wakurugenzi katika halmashauri hizo kusimamia vyema miundombinu ya michezo na kuhakikisha maeneo ya michezo hayavamiwi.
“Nawaagiza walimu wakuu wa shule zote nchini, kusimamia vyema vipindi vya michezo kwa kuhakikisha somo hilo linafundishwa kwani limeruhusiwa kuwepo kwenye mitaala na katika muda sahihi na wanafunzi wanashiriki vyema vipindi vya michezo. Na sisi upande wa Serikali tutasimamia vyema ajenda hiyo na tutahakikisha maafisa elimu Mkoa na Wilaya wanafuatilia michezo katika maeneo yao, ” Jafo.
Kwa upande wake Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako amesema kuwa Wizara yake itahakikisha inakamilisha uandaaji wa michepuo ya masomo ya michezo na kuhuisha mitaala iliyopo katika somo la michezo ili somo hilo lilete tija kwa wanafunzi ambao baadhi wameanza kulifanyia mitihani katika kidato cha nne na sasa taratibu zinakamilishwa ili masomo hayo yaendelee hadi kidato cha tano na sita ili nchi ipate wataalamu wengi zaidi.
Naye Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa mbali na kuzishukuru Wizara hizo kushiriki na kutoa mawazo chanya yanayolenga kuboresha maendeleo ya michezo nchini, amesema dhamira ya Serikali ni kuleta uhai katika timu za Taifa na uhai huo unatokana na kuwepo kwa vipaji vinavyozalishwa kuanzia shule za msingi na sekondari.