Imeelezwa kuwa Shule ya Sekondari ya JITEGEMEE (JKT) imeendaa mpango wa kuchangisha fedha unaolenga kukusanya zaidi ya Tsh, ml 600 kuelekea katika maadhimisho ya miaka 50, Shule ya Sekondari ya JITEGEMEE (JKT).
Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo, Kanali Robert Kessy, amebainisha hayo leo wakati wa mkutano na waandishi wa habari, huku akielezea uchakavu wa miundombinu hususani ya vyumba vya madarasa, majengo ya utawala na maabara kuwa ndiyo chanzo cha kampeni hiyo.
“Tunapoelekea Septemba 27, tarehe ya kuadhimisha miaka 50 ya shule yetu tangu kuanzishwa kwake, tunawakaribisha wadau mbalimbali wa elimu kuchangia katika kuimarisha vifaa vyetu,” alisema Kanali Kessy.
Hata hivyo Kanali Kessy alieleza shughuli za ziada zilizopangwa katika kuelekea maadhimisho hayo, ikiwa ni pamoja na kuwafikia wananchi wa pembezoni na kampeni za usafishaji mazingira ili kuendeleza juhudi za uhifadhi nchi nzima.