Zaidi ya watu 70 wanakisiwa kuuawa katika shambulio la kundi lenye uhusiano na al-Qaeda kwenye mji mkuu wa Mali Bamako mapema wiki hii, kulingana na vyanzo vya kidiplomasia na usalama.
Wapiganaji wenye misimamo mikali kutoka Jama’at Nusrat al-Islam wa al-Muslimeen (JNIM) walifanya shambulizi dhidi ya chuo cha mafunzo ya polisi na uwanja wa ndege wa karibu siku ya Jumanne, na kusababisha mshtuko na hasira katika nchi hiyo ya Afrika Magharibi.
Chanzo cha usalama kilichozungumza kwa sharti la kutotajwa jina, kiliambia shirika la habari la AFP kuwa watu 77 wameuawa na 255 kujeruhiwa katika shambulio hilo.
Hati rasmi ya siri iliyoidhinishwa iliweka idadi ya vifo kuwa takriban 100, na kubaini wahasiriwa 81, AFP iliongeza.
Wanadiplomasia wawili wanaohudumu katika eneo hilo, akiwemo mmoja aliyeko Bamako, waliambia shirika la habari la Reuters kwamba idadi ya waliofariki inaaminika kuwa katika miaka ya 70.
Mwanadiplomasia wa tatu anayeishi katika kanda hiyo alisema mamia wanaaminika kufariki na kujeruhiwa, na hospitali zimekosa vitanda kuwatibu waathiriwa.