Ikiwa katika maadhimisho ya miaka 30 tokea kuanzishwa kwake, Benki ya CRDB imetangaza mafanikio makubwa ya hatifungani ya miundombinu ya ‘Samia Infrastructure Bond,’ ambayo imevuka lengo kwa asilimia 115, ikikusanya Shilingi bilioni 323 – zaidi ya mara mbili ya lengo lake la awali la kukusanya Shilingi bilioni 150.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa ameipongeza Benki ya CRDB kwa mafanikio makubwa ya mauzo ya Hatifungani ya Samia Infrastructure Bond iliyokusanya TZS bilioni 323 ambazo ni zaidi ya mara mbili ya lengo la awali la kupata TZS bilioni 150.
Mafanikio haya yaliyopatikana ndani ya mwezi mmoja na nusu wa mauzo hayo yanaonyesha imani kubwa waliyonayo wawekezaji kwa Benki ya CRDB hali inayoiweka mahali pazuri zaidi kuimarisha nafasi yake kama benki kinara katika sekta ya fedha nchini.
Hatifungani hii iliyotajwa kwa heshima ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, inaonyesha dhamira ya Benki ya CRDB kuchangia kukuza uchumi wa taifa na kuimarisha kipato cha mwananchi mmojammoja.
Kupitia fedha zilizokusanywa baada ya mauzo ya hatifungani hii, wananchi watanufaika kutokana na ukamilishaji kwa wakati wa utekelezaji wa ujenzi wa miundombinu ya barabara za mijini na vijijini.
Mheshimiwa Mchengerwa amesifu mafanikio haya akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP) katika kuboresha miundombinu ya usafiri na kukabiliana na changamoto zinazowakabili wananchi, wafanyabiashara na wawekezaji nchini.
“Hatifungani ya Samia Infrastructure Bond ni mfano halisi wa namna ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi unavyoweza kuleta manufaa kwa taifa letu. Kiasi hiki cha TZS 323 bilioni kilichokusanywa kinatoa mwanga wenye matumaini kwa maendeleo ya miundombinu hasa ya barabara huko mbeleni.
Nawapongeza sana Benki ya CRDB kwa ubunifu huu mliokuja nao katika kuisaidia serikali kukamilisha mipango yake ya kuboresha maisha ya wananchi,” amesema Waziri Mchengerwa.
Kwa zaidi ya mwezi mmoja na nusu tangu tarehe 29 Novemba 2024 uzinduzi wa mauzo hayo ulipofanyika mpaka Januari 17 dirisha hilo lilipofungwa, kampuni na taasisi 327 zimejitokeza kuwekeza zaidi ya TZS 118.99 bilioni pamoja na watu binafsi 6,896 waliowekeza jumla ya TZS 204.1 bilioni. Asilimia 94 ya kiasi chot ekilichopatikana kimekusanywa kupitia Programu ya SimBanking.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela amesema mafanikio yaliyoyapata yanadhihirisha ukubwa nauwezo wa uwekezaji walionao wananchi pamoja na kampuni zilizopo katika soko letu sambamba na utayari wao kuwekeza hasa wanapojiridhisha na uhakika wa mradi na Benki ya CRDB inajisikia fahari kubwa kuaminiwa na Watanzania kwa ujumla wao.
Kazi kubwa iliyofanywa na menejimenti ya Benki ya CRDB ikishirikiana na Wizara ya TAMISEMI kupitia Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) amesema imekuwa na mafanikio makubwa ambayo matunda yake yatawanufaisha Watanzania wengi. “Tumepata wawekezaji wengi binafsi kwa sababu walimudu kiwango cha chini cha shilingi 500,000 tu.
Fedha zote tulizozikusanya kwenye mauzo ya hatifungani ya Samia Infrastructure Bond zitatumika kuwawezesha makandarasi wa wanaotekeleza na watakaoshinda zabuni zitakazotangazwa na TARURA. Tunaamini upatikanaji wa fedha hizi utasaidia kwa kiasi kikubwa kukamilisha miradi kwa wakati,” amesema Nsekela.
Wawekezaji hawa, Nsekela amesema wataendelea kushirikiana nao kwa kipindi chote cha miaka mitano ya uhai wa hatifungani hii kama walivyowaahidi wakati wa mauzo yaliyofanyika nchi nzima ikiwamo kulipa riba ya asilimia 12 kwa mwaka itakayotolewa kwa awamu nne. “Malipo ya riba yatakuwa yanafanyika kila tarehe 10 Februari, 10 Mei, 10 Agosti, na 10 Novemba. Kwa mwaka huu, wataanza kupokea malipo ya faida tarehe 10 Mei,” amesema Nsekela.
Hatifungani ya Samia Infrastructure Bond ni awamu ya pili ya Mpango wa Muda wa Kati wa Miaka Mitano kwa ajili ya kukusanya Shilingi za Kitanzania sawa na Dola za Marekani Milioni 300 ambao uliridhiwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Masoko ya Fedha na Mitaji (CMSA) mwaka 2023.
Kupitia mpango huo, mwaka 2023 Benki ya CRDB ilikuwa ya kwanza nchini kuzindua hatifungani ya kijani iliyopewa jina la ‘Kijani Bond’, ambayo ilikuwa hatifungani ya kwanza kwa ukubwa kusini mwa Jangwa la Sahara. “Kijani Bond ilikuwa ni awamu ya kwanza ya mauzo ya Mpango wa Muda wa Kati wa Miaka Mitano na Samia Infrastructure Bond ni awamu ya pili ya mpango huo.
Kama tulivyovuka lengo katika mauzo ya Hatifungani ya Samia Infrastructure Bond, hali ilikuwa hivyo pia kwenye Kijani Bond iliyotuwezesha kukusanya shilingi bilioni 171.82 kutoka shilingi bilioni 40 zilizokusudiwa sawa na ufanisi wa asilimia 429.6,” amefafanua Nsekela.
Mkurugenzi Mtendaji wa TARURA, Mhandisi Victor Seff amesema ushirikiano huu ulioanzishwa kati ya Benki ya CRDB na TARURA utakuwa na manufaa makubwa katika utekelezaji wa miradi ya barabara nchini. “Tunayo miradi mingi inayotekelezwa katika maeneo tofauti nchini na changamoto kubwa iliyokuwepo ilikuwa upatikanaji wa fedha kwa ajili ya malipo ya makandarasi. Naamini wengi sasa watapata fedha zao kwa wakati ili kukamilisha miradi kwa muda uliopangwa,” amesema Mhandisi Seff.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa CMSA, CPA Nicodemus Mkama alisema kuwa kuorodheshwa kwa Samia Infrastructure Bond kumetongeza thamani ya uwekezaji katika hatifungani za kampuni na taasisi kwa asilimia 38.9, na kufikia TZS trilioni 1.16 kutoka TZS bilioni 837.31.
“Samia Infrastructure Bond ni kielelezo wazi cha nguvu za masoko yetu ya mitaji, na kuufanya Soko la Hisa la Dar es Salaam kuwa mchezaji muhimu katika kuwezesha uwekezaji katika miradi ya miundombinu ya kitaifa ya Tanzania,” aliongeza Bwana Mkama.
Baada ya kutangaza matokeo ya mauzo, hatifungani hiyo iliorodheshwa Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE) ili kuwaruhusu wawekezaji waliochelewa kupata nafasi ya kushiriki kuijenga nchi yao huku wakipata faida ya asilimia 12 itakayotolewa kwa kipindi chote cha miaka mitano.
Afisa Mtendaji Mkuu wa DSE, Peter Nalitolela amesema kila siku idadi ya Watanzania wanaoshiriki sokoni hapo inazidi kuongezeka jambo linalotia matumaini kwamba litazidi kukua hivyo kuwa na manufaa makubwa hapo siku za mbeleni. “Mafanikio zinazopata makampuni yaiyoorodheshwa sokoni ni mfanikio ya soko zima.
Sisi wasimamizi wa soko tunapata faraja kuona mambo yanaenda vizuri kila kunapokuwa na bidhaa mfano wa Hatifungani hii ya Samia Infrastructure Bond ya Benki ya CRDB,” amesema Nalitolela.