Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) inaungana na Shirika la Miliki Ubunifu Duniani (WIPO) na nchi nyingine kuadhimisha siku ya Miliki Ubunifu Duniani ambayo huadhimishwa Aprili, 26 kila mwaka.
Lengo la maadhimisho haya ni kukuza Vumbuzi na Bunifu mbalimbali kwa manufaa ya baadaye na kutambua mchango wa ubunifu katika kufikia maendelea endelevu.
Maadhimisho haya kwa Tanzania yatafanyika tarehe 09 Mei 2024 na yanatarajiwa kuwa na ushiriki wa Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), Waziri wa Viwanda na Biashara ambaye ndiye Mratibu wa shughuli hii, vilevile kutakuwa na ushiriki wa Hamis Mwinjuma (Mb), Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo.
Kauli mbiu ya maadhimisho ya siku ya Miliki Bunifu Duniani kwa mwaka 2024 ni “Miliki Ubunifu na Malengo ya Maendeleo Endelevu: Kujenga mustakabali wa pamoja kwa kutumia ubunifu (Intellectual Property and the SDGs: Building our Common further with.
Shirika la Miliki Ubunifu Duniani (WIPO), lilianzishwa kwa lengo la kukuza na kulinda nyenzo za Miliki Ubunifu ikiwemo vumbuzi kwa kutoa Hataza,alama zinazowekwa kwenye bidhaa na huduma, hakimiliki na hakishiriki.
Tanzania ni miongoni mwa nchi mwanachama wa WIPO, hivyo imekuwa ikiunga mkono na kushiriki katika jitihada zinazofanywa na shirika hilo kwa kuhakikisha kuwa inakuza uelewa wa masuala ya Miliki Ubunifu pamoja na kuzilinda kisheria ili kwenda sambamba na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia na kukuza uchumi.
Katika maadhimisho ya mwaka huu yatakayofanyika katika Hoteli ya Johari Rotana, Dar es Salaam, BRELA inawaalika wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na Taasisi zinazosimamia masuala ya Miliki Ubunifu Tanzania Bara na Zanzibar, Taasisi za umma pamoja na sekta binafsi ili kujadili kwa pamoja fursa, mafanikio na changamoto zilizopo katika nyanja ya Miliki Ubunifu.
Vilevile, baadhi ya wabunifu kutoka sekta mbalimbali watashiriki na kazi zao za ubunifu zitaoneshwa
Kuelekea maadhimisho haya, Maafisa wa BRELA na COSOTA wametoa elimu kuhusu Miliki Ubunifu katika baadhi ya Vyuo vya Elimu ya Juu, Vyuo vya Ufundi na Teknolojia, Waandishi wa Habari, Wazalishaji na Wajasiriamali.
Pamoja na kutoa elimu kupitia vyombo vya habari ikiwa ni njia mojawapo ya kuwahamasisha wabunifu kuhakikisha wanaendeleza na kulinda bunifu zao ili ziwapatie manufaa wao pamoja na Taifa kwa ujumla.
Matukio muhimu katika maadhimisho haya, ni pamoja na mijadala kuhusu Miliki Ubunifu ambayo itahusisha Sekta za Umma na Binafsi ambao kwa pamoja watajadili kuhusu fursa, mafanikio na changamoto wanazokutana nazo katika nyanja ya Miliki Ubunifu.
Vile vile, Hati za Makubaliano ya ushirikiano katika eneo la Miliki Ubunifu baina ya BRELA, COSOTA na Taasisi nyingine zitasainiwa ikiwa ni njia ya kurasimisha ushirikiano uliopo baina ya Taasisi hizo katika kuhakikisha Miliki Ubunifu inaleta manufaa katika maendeleo ya kiuchumi na teknolojia nchini.